Jamhuri ya Muungano wa Tanzania

OFISI YA MSAJILI WA HAZINA

Taasisi za Umma zapitisha maazimio tisa ya kuimarisha ufanisi
16 Sep, 2025
Taasisi za Umma zapitisha maazimio tisa ya kuimarisha ufanisi

Na Mwandishi wa OMH

Dar es Salaam.  Zaidi ya Wenyeviti wa Bodi na Wakuu wa Taasisi za Umma 650 nchini walikutana jijini Arusha kati ya Agosti 23–26, 2025 katika kikao kazi cha mwaka, maarufu kama, CEOs Forum, na kukubaliana juu ya maazimio tisa yanayolenga kuimarisha ufanisi wa taasisi za umma, kuongeza tija na kupunguza utegemezi kwa Serikali.

 

Miongoni mwa maazimio hayo ni kuimarisha usimamizi wa rasilimali za umma kwa kudhibiti matumizi na kuongeza ubunifu, pamoja na kusisitiza uwekezaji zaidi katika tafiti ili kusaidia maamuzi yanayotegemea ushahidi wa kitaalamu.

 

Aidha, taasisi hizo zimekubaliana kufanya mapitio ya sera na sheria zinazosimamia shughuli zao, ili kubaini changamoto zilizopo na kutoa mapendekezo ya maboresho.

 

Katika azimio lingine, kikao kimezitaka taasisi kuanza kujijengea uwezo wa kuripoti masuala ya Mazingira, Kijamii na Utawala “Sustainability – ESG” kuanzia mwaka wa fedha 2025/26, kulingana na miongozo iliyopo.

 

Pia, kikao kiliazimia taasisi na mashirika ya umma kuweka mikakati mahsusi na thabiti ya utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, huku mamlaka zinazoratibu matumizi ya TEHAMA zikihimizwa kufanya tathmini ili kupunguza uthibiti kupita kiasi na kuruhusu ubunifu katika matumizi ya teknolojia.

 

Kwa upande wake, Ofisi ya Msajili wa Hazina imepewa jukumu la kuendelea kuboresha vigezo vya kutambua mashirika yenye utendaji bora, ikiwemo yale yasiyo ya kibiashara.

 

Katika maazimio mengine, mashirika ya umma yameshauriwa kuendeleza maboresho ya kimfumo kwa lengo la kupunguza utegemezi katika Mfuko Mkuu wa Serikali.

 

Kikao hicho pia kilipendekeza jina la mkutano huo libadilishwe kutoka CEOs Forum na kuwa C-CEOs Forum kuanzia mwaka wa 2026/27, ili kuakisi wahusika wakuu wa mkutano ambao ni Wenyeviti wa Bodi na Watendaji Wakuu wa Taasisi.