Na Mwandishi Maalumu,
KATIKA kuhakikisha watumishi wake wanakuwa na afya bora na kuboresha mahusiano mahali pa kazi, Ofisi ya Msajili wa Hazina jana ilifanya Bonanza kubwa kwa ajili ya watumishi wake lililofanyika Viwanja vya Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT), Jijini Dar es Salaam.
Zaidi ya wanamichezo 100 walifurahia Bonanza hilo lililoshirikisha mazoezi ya viungo, mpira wa miguu, kuvuta kamba, riadha, mbio za magunia na kukimbiza kuku.
Akizungumza wakati wa kuhitimisha bonanza hilo, Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu katika Ofisi ya Msajili wa Hazina, Pili Mazowea aliyekuwa mgeni rasmi akimwakilisha Msajili wa Hazina, Mgonya Benedicto, alisema lengo kuu la Bonanza hilo ni kuimarisha afya ya watumishi na kuboresha mahusiano mahali pa kazi.
Aliongeza kuwa, afya ikiwa nzuri kwa watumishi hata utendaji kazi unakuwa mzuri, hivyo amewasihi kushiriki michezo mara kwa mara ili kuimarisha afya.
Aliwapongeza pia watumishi walioshiriki katika bonanza hilo kwa kujitokeza kwa wingi, akiamini watakuwa mabalozi wazuri kwa wengine katika kutunza afya zao kupitia michezo.
Washindi wa michezo mbalimbali walizawadiwa vikombe huku washiriki wakitunukiwa medali.
Hilo lilikuwa bonanza la pili kwa watumishi wa Ofisi ya Msajili wa Hazina kufanyika kati ya mwaka jana na mwaka huu na kwanza aina hiyo ya kusanyiko la kimichezo litakuwa endelevu.